WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amepiga marufuku matumizi ya viberiti,
mishumaa na hita za kuchemshia maji kwa wanafunzi wa bweni ili kuepusha
majanga ya moto na atakayekutwa, atachukuliwa hatua kali.
“Kuna tabia ya baadhi ya wanafunzi hasa wa masomo ya fizikia kutengeneza
vifaa vya kienyeji vya kuchemsha maji mabwenini, jambo hili ni la
hatari kwani linaweza kusababisha ajali ya moto, hivyo ni marukufu kwa
mwanafunzi kutumia vifaa hivyo,” alisema.
Waziri Mkuu alitoa agizo hilo jana katika harambee ya kuchangisha fedha
za ujenzi wa majengo ya Shule ya Sekondari Lindi, yaliyoungua moto usiku
wa kuamkia Julai 10, mwaka huu.
Katika ajali hiyo shule imeathirika kwa asilimia 34 baada ya vyumba tisa
vya madarasa, jengo lenye matundu 26 ya vyoo na jengo la maabara ya
kemia na fizikia yameungua na kusababishia hasara ya Sh milioni 682.78.
Waziri Mkuu alisema kwa namna ambavyo majengo hayo yameungua, ni vema
yakavunjwa na kujengwa upya. Aliwataka kutumia nafasi hiyo kujenga jengo
la ghorofa ili kutumia eneo dogo kwa kujenga madarasa mengi.
Pia alimuagiza Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi kuhakikisha fedha
zitakazopatikana katika harambee hiyo, zinatumika kama ilivyokusudiwa.
Harambee ilihudhuriwa na mke wa Waziri Mkuu, Mary Majaliwa, mke wa Rais
mstaafu wa Awamu ya Nne, Mama Salma Kikwete, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara,
Halima Dendego na wadau wa maendeleo na wanafunzi waliosoma shule hiyo
akiwemo Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Ramo Makani.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amezitaka taasisi mbalimbali nchini
kufunga vifaa vya kuzimia moto katika majengo yao kwa ajili ya kuvitumia
pindi ajali za moto zinapotokea
Post a Comment